Wasiliana Nasi

Wasiliana Nasi

Wednesday, March 25, 2015

MUME ALIVYOMFANYIA UKATILI MKEWE

Na Hamida Hassan
HUU ni ukatili uliopitiliza! Mwanamke mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Neema Mwita, anateseka katika Hospitali ya Mkoa wa Mara kufuatia jereha kubwa alilopata baada ya mumewe aliyemtaja kwa jina la Juma Mwita kummwagia uji wa moto kisa kikiwa ni kuchuma mahindi shambani bila ridhaa ya mumewe huyo.Akizungumza na Uwazi huku akimwaga machozi kila wakati, mwanamke huyo alisema siku ya tukio, yeye na mumewe walikuwa kazini na mwanaume huyo ambaye alipata tenda kubwa ya kufyatua matofali.


Neema Mwita akihojiwa.

MSIKIE MWENYEWE
“Nilikuwa nakusanya majani. Baada ya kukusanya kwa muda mrefu ambapo niliagizwa na mume wangu, niliamua kwenda shambani kuchuma mahindi kisha nikarudi nyumbani kupika chakula cha mchana ili akitoka kazini ale.

“Nikiwa jikoni nasubiri uji uchemke ili nisonge ugali, mume wangu alirudi ghafla na kuanza kunigombeza eti kwa nini nilichuma mahindi shambani na nilirudi nyumbani bila ridhaa yake?” alisema na kuanza kulia.

MUME ACHUKUA UJI WA UGALI
Mwanamke huyo aliendelea kusema: “Alinihoji ni kazi gani kubwa niliyoifanya kule kwenye matofali mpaka nikaamua kurudi nyumbani. Kabla sijajibu aliifuata sufuria yenye uji unaochemka jikoni na kunimwagia ambapo ulitua kifuani kwangu na kuniunguza vibaya, kama unavyoona. Sijajua mume wangu alikusudia nini kunifanya hivi!”

JIRANI AMWOKOA
Mwanamke huyo aliendelea kusema kuwa, baada ya kumwagiwa uji huo na kuungua, alianguka chini na kulia kwa maumivu, ndipo jirani yake mmoja alimwona akihangaika na kumchukua hadi ndani.

AKAA NYUMBANI SIKU SABA
“Ndani nilikaa kwa wiki nzima, maumivu yalikuwa makali sana. Ndipo wazazi wangu walipopata taarifa wakaja kunichukua. Hata hivyo, wazazi wangu nao hawakunipeleka hospitali, waliniweka nyumbani na kuniletea mganga wa kienyeji.”


Mwandishi akizidi kumuhoji Neema Mwita.

MUME AKIMBILIA KUSIKOJULIKANA
Neema alisema mumewe aliyeoana naye kwa upendo na kiapo cha kuishi katika shida na raha mpaka kufa, alikimbia baada ya tukio hilo na hajawahi kuonekana mpaka sasa ambapo polisi wanaendelea kumsaka usiku na mchana.

TAARIFA ZINAFIKA SERIKALINI
Mwanamke huyo ambaye kutokana na kuungua huko mishipa yake ya sehemu ya kidevuni imeshikana na ya shingo, alisema baada ya wiki moja, taarifa zilimfikia Mwenyekiti wa Kijiji cha Nyamisanga, Boke Chacha ambaye alimchukua mikononi mwa wazazi hao na kumpeleka hospitali kwa matibabu.

LICHA YA KUUNGUA, AMETELEKEZWA
Neema, anasikitisha sana kwani licha ya kupitia kipindi hicho kigumu, anadai ametelekezwa na wazazi wake na mtu anayemsaidia ni mwanaye wa kiume anayeitwa Wambura Juma aliyekuwa akisoma kidato cha tano.
“Mtoto wangu huyu kwa sasa hasomi kwa sababu ya kunisaidia mimi, alilazimika kuacha masomo toka tukio hili liliponitokea,” alisema Neema.

ANA MIEZI NANE HOSPITALINI
Neema anasema tangu alazwe hospitalini hapo, sasa ni mwezi wa nane lakini anamshukuru Mungu ameanza kujikongoja kutembea japo kwa taabu sana.

Muonekano wa jeraha alolipata Neema baada ya kuunguzwa na mumewe kwa uji wamoto.

MADHARA ALIYOYAPATA
Neema amepata madhara makubwa kufuatia tukio hilo kwani kwa sasa mkono wa kulia haukunjuki sawasawa kama zamani, hawezi kunyoosha shingo kutokana na nyama za shingo kuungana na kidevu, mdomo wake umepinda kidogo huku titi la upande wa kulia likiwa halipo tena!

APATIWA SIMU YA MKONONI
Joyce Kiria ni Mtangazaji wa Kipindi cha Wanawake Live kinachorushwa hewani na Runinga ya EATV, alimtembelea Neema hospitalini na kumpa msaada wa simu ya mkononi ili iwe rahisi kwa wale watakaojitokeza kutaka kumsaidia kwa ajili ya pesa za matibabu kutumia simu hiyo. ANAHITAJI MSAADA
Ndugu msomaji, Neema anahitaji msaada wako wa hali na mali. Kama utakuwa na chochote na umeguswa na maumivu yake, unaombwa kutumia mawasiliano yake 0656 151 072 au 0756 768 305

0 comments:

Post a Comment