Wasiliana Nasi

Wasiliana Nasi

Friday, March 6, 2015

MATATIZO KATIKA KORODANI ZA MWANAUME (TESTICULAR FAILURE)



Kazi ya korodani ni kuzalisha mbegu za kiume na homoni za kiume (Testosterone). Kwa hiyo korodani kushindwa kufanya kazi maana yake ni kushindwa kuzalisha mbegu na homoni za kiume.

Chanzo cha tatizo
Tatizo hili huwapata baadhi ya wanaume na chanzo chake ni kama vile matumizi ya baadhi ya dawa kwa muda mrefu mfano dawa kama Ketoconazole, glucocorticoids na dawa za usingizi hasa zile za kutuliza maumivu makali.

Pia yapo magonjwa yanayoshambulia korodani, mfano ugonjwa wa Mump ambao huambatana na kuvimba nyuma ya sikio na mashavu, maambukizi na maumivu ya korodani, kansa ya korodani na ugonjwa uitwao kitaalamu Hemochromatosis unaoambatana na mfumo wa damu. Kuumia korodani na kuzungukwa na mishipa ya damu pia ni mojawapo ya chanzo cha korodani kutozalisha mbegu za uzazi.

Mambo ya hatari yanayoweza kuharibu korodani ni shughuli zetu za kila siku na hizi husababisha kila siku korodani iumie taratibu.
Mfano kuendesha pikipiki kwa muda mrefu.
Vilevile uvutaji bangi na sigara unachangia tatizo hili.

Dalili za korodani kushindwa kufanya kazi
Mojawapo ya dalili hizi ni kutokuongezeka kwa ukubwa au urefu wa viungo vya uzazi, yaani uume na korodani zenyewe. Mwanaume kuwa na matiti makubwa, kukaa na mwanamke muda mrefu zaidi ya mwaka bila ya kumpa mimba, mwili kutoendelea vizuri hata ukila vizuri na kufanya mazoezi unaona mwili haujengeki. Pia kutokuwa na hamu ya tendo la ndoa au kupungukiwa na nguvu za kiume kwa kiasi kikubwa, kutoota nywele makwapani au sehemu za siri au kuota kwa kiasi kidogo sana.

Mabadiliko ya balehe kuendelea taratibu sana utakuwa umri unakuwa mkubwa lakini bado unakuwa kama mtoto, yaani baadhi ya viungo haviendelei mfano kuota ndevu, mabadiliko ya sauti na sehemu za siri.

Uchunguzi

Kwa watoto wachanga wenye matatizo haya viungo vyao vya uzazi huwa havieleweki kama ni vya kiume au vya kike, kadiri anavyoendelea kukua viungo vya uzazi huwa vidogo na wakati mwingine korodani zake huvimba yaani moja huwa kubwa kuliko nyingine.

Vipimo vingine ni vya mifupa ambapo X-ray huonyesha mifupa inakuwa myepesi na huvunjika yenyewe hasa kwa watoto na vijana.

Homoni zake huwa hazipo katika mpangilio mzuri ambapo hupishanapishana mfano Testosterone huwa chini lakini FSH na LG na Prolactin huwa juu. Kwa watu wazima kiwango cha homoni ya Testosterone hupungua taratibu kadiri umri unavyoongezeka hivyo ni vigumu kuthibitisha tatizo kwa watu wazima kwa kuzingatia kipimo kimoja.

Matibabu
Dawa za homoni ya Testosterone hutolewa kwa uangalifu mkubwa chini ya usimamizi wa daktari, matumizi ya kiholela husababisha tezi dume kuvimba kwa kasi, ongezeko la chembechembe nyekundu za damu mwilini isivyo kawaida, mabadiliko ya rehemu au Cholesterol kwenye ndevu, kutopata usingizi na akili kutokuwa sawa.

Kama utatumia dawa zisizo na Testosterone ukazingatia maelekezo ya daktari unaweza kurudi katika hali ya kawaida.

Tatizo likitokea kabla ya balehe, ukuaji wa mtoto husimama.

Ushauri
Ni vema endapo una matatizo hayo tuliyoyaelezea basi wahi hospitali ya mkoa na umuone daktari wa masuala ya uzazi kwa uchunguzi wa kina.

Epuka mambo yote tuliyoyaelezea kama ni vyanzo vya kuharibu korodani zako.

2 comments: