Wasiliana Nasi

Wasiliana Nasi

Wednesday, March 4, 2015

MSHITUKO WA MOYO (MYOCARDIAL INFARCTION) -2




Baada ya kueleza matatizo ya mshituko wa moyo wiki iliyopita katika safu hii, leo tutafafanua ugonjwa wa moyo unaosababishwa na simanzi kama vile kutengana na mke au mpenzi wa mtu.
Jina la ugonjwa huu kitaalamu huitwa broken heart syndrome na husababishwa na kudhoofika ghafla kwa misuli ya moyo kwa muda mfupi.
Ugonjwa huu hauhusiani kabisa na tatizo la kukosekana kwa damu ya kutosha katika moyo.
Tatizo hili hujulikana kama broken heart syndrome kwa sababu hutokana na mtu kupata msiba wa mkewe/mumewe au mpenzi wake wa kudumu.
Lakini mgonjwa anaweza kuugua kutokana na kuwa na wasiwasi mara kwa mara kwa muda mrefu hali inayosababisha moyo kushindwa kufanya kazi  ghafla hali ambayo kitaalamu huitwa acute heart failure.
Kutokana na mgonjwa kuwa na wasiwasi anaweza kusababisha ugonjwa wa moyo kupiga bila mpangilio usio wa kawaida.
Dalili:
Dalili kubwa ya maradhi haya ni maumivu makali ya kifua na mgonjwa kupata matatizo ya upumuaji au kuhema kwa shida na uchovu pamoja na kusikia mapigo ya moyo yasiyo na mpangilio.
Ugonjwa huu husababishwa na mambo mengi kama ile mtu kupewa habari za kifo cha mke/mume au mpenzi wake wa karibu au kama anapewa taarifa kuwa ana maradhi kama vile ya saratani au Ukimwi.
Lakini pia mtu anaweza kupatwa na tatizo hili ikiwa atapata ugonjwa wa pumu, maambukizi, ajali ya gari au baada ya upasuaji mkubwa au kama amepoteza kiasi kikubwa cha fedha.
TIBA NA VIPIMO
Kuna vipimo vingi vya kugundua maradhi haya kama vile kile kiitwacho ECG, X-ray ya kifua, Echocardiogram kipimo cha damu kuangalia vimeng’enyo vya kwenye moyo na kadhalika.
Hakuna tiba ya madawa iliyo maalum kwa ajili ya kutibu ugonjwa huu japokuwa tiba yake inaweza kufanana na ile ya aliyepatwa na shambulio la moyo.
Daktari akishathibitisha kuwa mgonjwa ana broken heart syndrome anaweza kumpatia dawa kama vile zilizo katika kundi la angiotensin-converting enzyme (ACE) inhibitors mfano Benazapril, kundi la beta blockers kwa mfano carvedilol au kundi la diuretics kama vile frusemide (lasix). Dawa hizi husaidia kupunguza mzigo katika moyo na pia kuzuia usipate shambulio jipya.Kwa kawaida wagonjwa wengi hupata nafuu baada ya muda wa kama mwezi mmoja au miwili hivi.
Kinga
Hakuna dawa zilizothibitishwa zinazoweza kusaidia kuzuia hali hii isijitokeze ingawa matumizi ya muda mrefu ya dawa za kundi la beta blockers kama vile atenolol, carvedilol, au dawa zenye kuzuia uzalishaji wa homoni zenye kuchochea shinikizo katika moyo husaidia sana.

0 comments:

Post a Comment