Wasiliana Nasi

Wasiliana Nasi

Sunday, May 24, 2015

JOHARI AJIFUNGUA KWA SIRI

Brighton Masalu
Mshtuko! Baada ya kujulikana kwa wengi kuwa hana mtoto na madai ya kutokuwa na uwezo wa kuzaa, mwigizaji wa kitambo Bongo, Blandina William Chagula ‘Johari’ ameshangaza baada ya siri kuvuja kuwa amejifungua kwa siri ambapo mtoto ana umri wa miezi 7 sasa, jambo lililozua mkanganyiko na mjadala mzito, Risasi Jumamosi linakupa ‘exclusive story’.


Mwigizaji wa kitambo Bongo, Blandina William Chagula ‘Johari’

UBUYU WAMWAGWA
Mwandishi wetu akiwa katika majukumu yake ya kila siku, ghafla alipigiwa simu na chanzo chake cha kuaminika ambacho ni mtu wa karibu wa Johari na kuanika kila kitu huku kikiomba hifadhi ya jina.


Mtoto wa Johari.

Sosi: Wewe (kikitaja jina la mwandishi) una habari?
Mwandishi: Zimejaa tele lakini hiyo yako inaweza kuwa ya muhimu zaidi.
Sosi: Tena ni muhimu kweli, unajua kuwa Johari ana mtoto na sasa anatimiza miezi saba?
Mwandishi: Unasema? Kajifungua lini na wapi?
Sosi: Kitambo tu, mbona hata kwenye ukurasa wake wa Instagram kaweka hizo picha, kwani hamjaingia huko?
Mwandishi: Ok, ok, nashukuru kwa taarifa.

Chanzo hicho kilisema kuwa, Johari alinasa mimba mwezi Machi, mwaka jana na kufanya siri kwa kutoonekana mara kwa mara na ilipofikisha muda wa kujifungua yaani mwezi Desemba alikwenda kujifungulia nyumbani kwao, Kijiji cha Ngokolo mkoani Shinyanga.

Huko alikaa kwa muda wa miezi minne na kurudi Dar kwa siri ambapo mtoto alitafutiwa mlezi maalum akishirikiana na mama mzazi wa Johari (jina linahifadhiwa).
Wakati hayo yakiendelea, ilisemekana kwamba Johari alikuwa akipigana usiku na mchana kutunza siri hiyo ikiwemo kutoruhusu watu wengi wakiwemo jamaa na marafiki kufika nyumbani kwao, Ubungo, Dar.


Mwigizaji wa kitambo Bongo, Blandina William Chagula ‘Johari’ akiwa na mwanaye.

JOHARI ASAKWA KILA KONA
Baada ya mwanahabari wetu kupata ubuyu huo, alianza harakati za kumsaka Johari kwa njia ya simu ya kiganjani lakini hakupatikana na kuamua kwenda hadi ofisini kwake, Sinza-Mori jijini Dar.
Alipokutwa ofisini kwake, RJ, Johari alibanwa juu ya madai hayo ambapo awali, alikataa kwa kutikisa kichwa huku akisindikiza na maneno ya kutaka kuheshimiwa.

“Hakuna kitu kama hicho na kama huna kingine cha kuuliza, naomba uniache nina majukumu mengi mezani kwangu,” alisema Johari huku akimtazama mwandishi wetu kwa jicho la ‘niondolee umbeya wako hapa’ licha ya mwandishi wetu kubaini mabadiliko mwilini mwake ikiwemo kunawiri kulikopitiliza.

UCHUNGUZI ZAIDI
Mwandishi wetu hakuridhika na majibu ya msanii huyo ndipo akaamua kuingia kwa undani na kina zaidi kutafuta data za kutosha ili kujua lipi ni tui na yapi ni maziwa juu ya utata wa habari hiyo.

Mwanahabari wetu alianza kwa kuwapeleleza watu wa karibu wakiwemo wafanyakazi wenzake na kubahatika kupata maelezo ya kina zaidi kutoka kwa mmoja wa rafiki mwingine wa Johari na kuyalinganisha na yale ya sosi wa kwanza na kubaini ukweli halisi.
“Huyo (Johari) asiwadanganye kabisa, ukweli ni kwamba alijifungua mwezi Desemba, mwaka jana kuelekea Krismasi na alikwenda kujifungulia kwao Shinyanga.

RISASI LAMRUDIA JOHARI
Kama mjumbe wa nyumba kumi, mwandishi wetu hakuchoka hivyo aliamua kumtafuta tena Johari huku safari hii akitumia mbinu za ndani za taaluma yake (uandishi) ambapo alimtega Johari kuwa anamhitaji kwa shida nyingine na kuomba miadi (appointment) ya kukutana naye.


Johari akiwa na mwanaye katika picha tofauti.

AINGIA, ATOKA!
Katika kupanga mahali na wakati wa kuonana, huku mwandishi wetu akiwa na ushahidi wa picha zikimuonesha Johari akiwa na mtoto wake na nyingine zikimuonesha mama yake Johari akiwa na mjukuu wake.

Hata hivyo, msanii huyo alileta upinzani mkali wa kukutana na mwandishi wetu na wakati mwingine kukubali kwa masharti mazito ikiwemo kutokuwa na kamera wala kifaa chochote cha kurekodia sauti, kitendo ambacho huitwa na vijana wa mjini kuingia na kutoka.

AWEKWA CHINI YA ULINZI
Baada ya vuta nikuvute ya muda mrefu, hatimaye walikubaliana kukutana Sinza-Mori na kuanza mazungumzo huku mwandishi akimuanzia mbali kabisa kwa kutumia saikolojia ya kiuandishi na bila kujishtukia, ghafla Johari alijikuta akiingia mwenyewe kwenye mtego na kujikuta akikiri kuwa amezaa na mtoto ana umri wa miezi saba sasa!

AWA MDOGO KAMA PIRITONI
Kwa kubanwa na maswali mazito na muhimu, Johari alijikuta akiwa mpole na mdogo mithili ya kidonge cha piritoni na kuamua kuweka wazi kila kitu licha ya kutumia mbinu za ‘mfamaji’.
“Lakini jamani, mimi si mwanamke? Sasa kama ni hivyo kuzaa ni jambo la ajabu au mlitaka niutangazie ulimwengu wote kuwa nimebeba mimba na sasa nimezaa?” alihoji Johari.

JINA LA MTOTO LAFANANA NA LA MAMA RAY!
Huku akimkazia macho usoni, ‘karani’ wetu alimuuliza Johari jina la ‘anko’ wake ambapo kwa uso uliochoka, msanii huyo alilitaja kuwa anaitwa Maria na ndipo mwandishi wetu akaibua swali jipya!

NI MTOTO WA RAY?
Mwandishi alishtuka kusikia jina la anko wake kwani hata mama mzazi wa aliyewahi kudaiwa kuwa mwandani wake ambaye ni mkurugenzi mwenzake Johari, Vincent Kigosi ‘Ray’ anaitwa Maria Kigosi.
Mwandishi: Kwani ni mtoto wa Ray?
Johari: (akikunja ndita) achana na mimi, nina kazi nyingine siko tayari kuendelea na mazungumzo.

HUKO NYUMA
Kabla ya ishu hii kuwa wazi, siku za nyuma Magazeti ya Global yaliwahi kunyetishiwa juu ya Johari kuwa mjamzito lakini alipoulizwa alikataa katakata. Hata alipofuatwa nyumbani kwao alijificha ili asionekane na wanahabari wetu. Ili kujua baba wa mtoto, usicheze mbali na Magazeti ya Global.

0 comments:

Post a Comment