Wasiliana Nasi

Wasiliana Nasi

Monday, February 16, 2015

MKE ASIMULIA MAPYA SAKATA LA MAUAJI YA MTEJA WA GARI

Haruni Sanchawa na Shani Ramadhani/Uwazi

LILE sakata la mauaji ya mteja wa gari aliyekutwa amefukiwa katika nyumba moja Ilala Sharifu Shamba jijini Dar, Farahan Habusali Maluli (31) limeingia katika sura mpya baada ya mkewe, Tatu Ally (29) kuelezea mambo mapya juu ya tukio hilo la kusikitisha.


...Mtuhumiwa akiwa chini ya ulinzi.

Akizungumza na Uwazi juzi nyumbani kwake, Maramba Mawili, Kinondoni, Dar, Tatu alisema mumewe alikuwa wakala mkuu wa mabasi ya Waiders yanayofanya safari zake kati ya Dar na Mtwara.

MARA YA MWISHO KUMUONA
Juni, mwaka jana ambayo ilikuwa mara yake ya mwisho kumuona marehemu, waliondoka wote nyumbani. Mume alikuwa akienda kazini yeye alikuwa akienda Kigamboni kwa wazazi wake.
“Tulipoachana mbele ya safari, mume wangu aliniambia niwahi kurudi nyumbani, tukakubaliana.”

AMPIGIA SIMU, HAPATIKANI!
Mwanamke huyo alizidi kusimulia: “Nilipomaliza shida ya Kigamboni nikiwa narudi nilimpigia simu kumfahamisha, lakini simu yake haikuwa hewani. Baada ya kupita saa tatu ikawa inapatikana, lakini nilipopiga haikupokelewa.
“Jambo hilo lilinitia wasiwasi, nikaanza kuwasiliana na ndugu zake kuwaeleza kwa sababu haikuwa kawaida yake kutopokea simu au isiwe hewani.”

FAMILIA YAANZA KUFUATILIA
“Baadaye jitihada za kifamilia zilianza ili kumtafuta, wakajaribu kwenye simu hali ikawa vilevile. Mwishowe tukaamua kwenda kutoa taarifa Kituo cha Polisi Mbezi Luis (Dar) kwa kufungua jalada la uchunguzi namba KMR/RB/47/2014 UCHUNGUZI.”


...Mwili ukifukuliwa.

MKE APIGIWA SIMU
“Baada ya siku kadhaa kupita, mtu mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Juma, alinipigia simu na kuniuliza kama mimi ndiye mke wa Farahan, nilipokubali, aliniambia mume wangu wanamshikilia kwa vile wanamdai shilingi milioni 75 ambazo zilitakiwa zitolewe ili aachiwe, vinginevyo wangempeleka kwa mkubwa wao (hawakusema wapi).

“Nilishangaa sana kusikia mume wangu anadaiwa kwa sababu aliwahi kuniambia hataki kudaiwa kwani madeni ni mabaya. Hata hivyo, niliwaomba wamuachie huru kwani wakati huo nilikuwa na kichanga cha mwezi mmoja.
“Nilimwambia kaka yake kuhusu mtu huyo, yeye alipompigia alimwambia hivyohivyo. Tuliipeleka ile namba polisi lakini wakatuambia mitandao si mizuri hivyo tuvumilie kusubiri uchunguzi wao.”



SIKU YA KUJUA UKWELI
“Sasa hivi karibuni nilipokuwa naangalia taarifa ya habari ya TV, nilishtuka kumuona mtu niliyemuona polisi akihusishwa na tukio la kupotea kwa mume wangu akiwa anapanda gari la polisi, nguvu ziliniishia, nilijaribu kuwasiliana na mashemeji zangu, wakaniambia nitulie.
“Baadaye nikaambiwa na mashemeji zangu kwamba mwili wa mume wangu umefukuliwa huko Ilala ndipo nikajua kumbe mtu yule niliyemuona kwenye TV ndiye alihusika.”

NANI ALIJUA?
Kwa mujibu wa mashuhuda, siri za kubainika kuwepo kwa kaburi ndani ya nyumba zilitokana na vijana wa mtaani waliopewa kazi ya kuchimba shimo alilofukiwa marehemu. Vijana hao walisema mtuhumiwa aliwaambia ni shimo kwa ajili ya kutapisha choo.


Siku ya ndoa yake marehemu.

Vijana hao hata hivyo, walisema walishangazwa kuona shimo hilo likichimbwa mbele ya nyumba badala ya nyuma kama ilivyozoeleka.
“Inadaiwa kabla ya kuchimba, jamaa aliwasiliana na mwenye nyumba juu ya nia yake ya kuchimba shimo hilo ili asishtuke akimkuta na alipomwambia akampa ruhusa lakini kwa sharti kuwa gharama hizo hazitamhusu mwenye nyumba huyo,” alisema shuhuda aliyezungumza na gazeti hili.

MAREHEMU ALIUAWA VIPI?
Kwa mujibu wa chanzo kilicho karibu na familia ambacho kilipata matokeo ya uchunguzi wa mwili uliofukuliwa, inaonesha kifo hicho kilitokea baada ya marehemu kunyongwa.



Muonekano wa shimo baada ya kufukiwa.

Katika hali ya kusikitisha, shuhuda huyo alisema shimo hilo baada ya kuchimbwa lilibaki wazi kwa siku mbili jambo linalodhihirisha kuwa mwili huo ulihifadhiwa ndani ya nyumba wakati mtuhumiwa akitafuta upenyo wa kutekeleza tendo hilo.

MKE WA MAREHEMU AITWA KUTAMBUA
Siku ya tukio la kufukuliwa kwa mwili huo ilibidi mke wa marehemu aitwe ili kuzitambua nguo ambazo mumewe alizivaa mara ya mwisho na alikiri ni zenyewe.

Akizungumzia tukio hilo, kaka wa marehemu aliyekataa jina lake kuandikwa gazetini, alisema walipata simu kutoka Kituo cha Polisi Mbezi Luis ya kuitwa na walipofika waliambiwa wawe wavumilivu, kwani ndugu yao aliyepotea kwa muda mrefu alikuwa ameuawa.


Polisi wakiwa eneo la tukio.

Tuliambiwa mdogo wetu hakupotea, bali aliuawa na kuzikwa katika nyumba moja Sharifu Shamba, tukaanza safari, tulipofika na kufukua, mkewe alikuja kuthibitisha nguo alizovaa,” alisema kaka huyo.
Anayehusishwa na tukio hilo ni Hemed Hamis (27) anayedaiwa kupewa na marehemu kiasi cha shilingi milioni 35 kwa ajili ya kumnunulia gari aina ya Fuso ya kubebea mchanga.

0 comments:

Post a Comment