Wasiliana Nasi

Wasiliana Nasi

Friday, April 18, 2014

MATATIZO YA KUPATA HAJA KUBWA AU KUCHELEWA KUPATA CHOO (CONSTIPATION)


Ni nini tatizo la kupata haja kubwa?
Ni  haja kubwa inayopatikana isiyozidi mara tatu katika wiki na ama haja kubwa inayoleta shida kutoka kwake na utokaji wake ni mithili ya mavi ya mbuzi (uyabisi) hata kama inapatikana kila siku. Hali hii inaposhamiri muathirika hupata choo si zaidi ya mara tatu katika kipindi cha  mwezi mmoja.
Ni moja miongoni mwa matatizo katika mfumo wa kusaga chakula yanayowakumba watu wengi si hapa kwetu Zanzibar tu bali dunia nzima kwa jumla. Shida ya kupata choo ni hali inayowakabili watu mbalimbali.


Dr. Fadhili Emily
Takriban ni wastan wa asilimia kumi na mbili ya watu duniani wanasadikiwa kuwa na tatizo la kuchelewa kupata haja kubwa. Katika hali ya kawaida mwanadamu hupata haja kubwa karibu kila siku au kila baada ya siku moja.
Kwa mtoto mchanga baada kuzaliwa huenda haja mara nne hadi tano kwa siku. Wale wanaonyonya maziwa ya mama (maziwa ya kifua) hupata haja mara nyingi zaidi ukilinganisha na wenzao wanaonyonya maziwa ya kopo yaani fomula (formula). Kwani baadhi yao hupata haja kila baada ya kunyonya wakati wenzao wa maziwa ya kopo hupata haja mara moja tu kwa kila baada siku mbili hadi tatu. Mtoto anaenyonya maziwa ya mama si aghlabu kupata shida ya haja kubwa. Anapotimiza umri wa miaka miwili mtoto hupata choo takriban mara moja hadi mbili kwa siku. Wakati mtoto wa umri wa miaka minne anapata haja kubwa mara moja kwa siku.
Jee hali ikoje hapa kwetu Zanzibar?
Katika kliniki zetu za upasuaji karibu asilimia kubwa ya wagonjwa wanaokuja kwa tatizo la kuumwa na tumbo wengi wao hubainika kuwa na hali isiyoridhisha katika masuala ya kupata haja kubwa. Aidha wagonjwa hao wamekuwa wakilalamika kuchelewa kupata au hupata haja kubwa kwa shida kabisa. Kwa watoto wachanga hali hii pia ipo, na kwa watu wazima kina mama husumbuliwa zaidi ukilinganisha na kina baba. Wazee nao hasa kwasababu ya umri ambapo maradhi mengi hujitokeza na pia kutoweza kujituma kama ilivyo kwa vijana, husumbuliwa na tatizo hili kwa kiasi kikubwa. Watu wengi wamekuwa wakijitibu wenyewe pasipo kujua nini hasa kinawasibu. Hali hiyo hupelekea kwa baadhi yao kupata madhara zaidi wasiyoyatarajia. Mathalan hupata vidonda vya tumbo, maumivu ya tumbo yasiokwisha, kuharisha mara kwa mara, na baadhi yao chango huziba hali inayowapelekea kufanyiwa opresheni ya dharura.
Kuchelewa kupata haja kubwa huwa ni sababu kuu ya kupata maumivu wakati wa kwenda haja. Hali inapokuwa mbaya mtu hukosa kabisa kupata choo na kujamba pia, na uchango wake mkubwa hujaa kinyesi. Kushindwa kupata haja kubwa ni dalili inayotokana na sababu nyingi. Sababu zenyewe zimejigawa namna mbili. Mosi, kuziba choo, na pili ni uchango kuwa na mwendo wa taratibu mno.
SABABU
Zipo sababu kadhaa zinazopelekea kutokea kwa tatizo la kukosa kupata haja kubwa kikawaida, miongoni mwa hizo ni kama hizi zifuatazo:
  • Inaweza ikawa yenyewe tu bila kusababishwa na hali yoyote ile kama vile madhara ya dawa
fulani, au hali ya kiafya, na huwa haiambatani na maumivu ya tumbo. Kwa lugha nyengine ni kwamba sababu hasa huwa haijulikani. Hii ndio sababu maarufu kuliko nyengine zote.
  • Inaweza kusababishwa na mpangilio mbaya wa chakula, kutokula vyakula vyenye fiber (nyuzinyuzi), kunywa maji kidogo kuliko inavyotakiwa.
  • Matumizi ya dawa mbalimbali na baadhi ya athari zake kama vile baadhi ya dawa za kutibu presha (shinikizo la damu), dawa za kupunguza maumivu, dawa za kutibu degedege, dawa za kutibu mamivu ya tumbo ikiwa pamoja na dawa za kutibu mfadhaiko, dawa za kutibu alaji (makole).
  • Mgonjwa wa maradhi ya kisukari, maradhi ya misuli.
  • Maradhi ya uvimbe katika uti wa mgongo, kansa ya utumbo mkubwa, kidonda/kuchanika njia ya haja kubwa mlangoni yaani fisha (anal fissure).
  • Kwa makusudi tu mtu hujizuwia asiende haja kwa sababu labda hakuna choo cha kuridhisha, anaogopa maumivu hasa wale wenye fisha (anal fissure), ama kwa uvivu tu.
  • Watoto nao hupata tatizo la kuzaliwa nalo. Kukosekana mishipa ya fahamu katika sehemu ya utumbo mkubwa huwa ndio sababu inayopelekea utumbo huo kutosukuma kinyesi hivyo kusababisha kuchelewa kupata haja kubwa ambapo mara nyengine hupindukia kipindi cha wiki moja hadi mbili au hata zaidi. Kwa maana hiyo tumbo huvimba na mtoto hudhoofu kiafya. Hili ni tatizo la kipekee.
VIPI TUNACHUNGUZA
Maelezo ama dalili mgonjwa anazozielezea jinsi anavyosumbuka kupata haja kubwa, pekee hutoa taswira kamili ya tatizo linalomkabili. Miongoni mwa dalili hizo ni zile pamoja na kuwa na choo kigumu, hutoka kwa shida, hufanana na mavi ya mbuzi ama sungura yaani uyabisi. Dalili nyengine ni mbweo, kuvimba tumbo, maumivu ya tumbo, kuumwa na kichwa, uchovu, kutojiskia vizuri na pia kuwa na hisia za kutomaliza haja yote. Na anapoulizwa mgonjwa juu ya mpangilio wake wa mlo mara nyingi hubainika kutokutumia vyakula vyenye nyuzinyuzi (hivi ni vyakula vya sehemu ya mimea ambayo haisagwi na mwili wetu na hivyo kusukuma utumbo, huku ikifyonza maji wakati ikitoka na kufanikisha kupata haja kubwa). Wengi wao hawali nafaka, mboga za majani, na matunda kama mlo wa kawaida. Kutokunywa maji ya kutosha, kutofanya mazoezi kikawaida au wakati mwengine husababishwa na matumizi ya baadhi ya dawa ambazo kwa kuzitumia kwa kipindi cha muda mrefu hatimae huleta athari ya kuzuwia au kuchelewa kupata choo.
Tunachunguza kwa kuliangalia na kugusa tumbo, ikibidi huangalia njia ya haja kubwa, wakati mwengine hata kwa kutumia darubini maalum tunaweza kubaini tatizo hilo. Xray ya tumbo ingawa si lazima, nayo pia huweza kutumika kubainisha uwepo wa tatizo.
KINGA
JE, VIPI TUNAWEZA KUJIKINGA?
Ni rahisi zaidi kukinga usipate hali hii kuliko kutibu. Mara au pindi ukipata nafuu jambo la msingi ni kujitahidi kuendeleza mazoezi kwa maana ya matembezi, kuogelea, au kushiriki michezo ya aina yoyote ile ilimradi tu utoke jasho. Kunywa maji kiasi cha kutosha ambacho kwa wastani mtu mzima anatakiwa kwa siku anywe lita mbili hadi mbili na nusu kulingana na hali ya hewa. Kula mboga za majani kama vile mchicha, kisambu, mtoriro, kabichi, karoti na nyenginezo; nafaka kwa mfano karanga, mahindi, ngano, fiwi, mbaazi, kunde, maharage, njugu mawe na kadhalika; pendelea kula matunda hususan ndizi mbivu, embe, chenza na machungwa (kula hadi maganda ya ndani), papai, balungi, pea(parachichi), fenesi, epul (usilimenye), shelisheli na mengine mengi tu ambayo kwa kweli katika mazingira yetu Mola ametujaalia tunayo mengi sihaba. Yote haya hutengeneza mazingira mazuri ya kupata haja kubwa kikawaida na bila shida yoyote.
Na kwa watoto ni kuwapangia muda wa kwenda kujisaidia mapema asubuhi na kipindi cha takriban dakika thelathini baada kupata mlo.
NINI HASA KAZI YA VYAKULA VYENYE NYUZINYUZI?
Vyakula vya namna hii kwa kawaida havisagwi na mwili kwahiyo hupita katika utumbo na kutoka mwilini.Iwapo tutakula nafaka na matunda na mboga za majani tutakuwa na nafasi kubwa kujikinga kupata maradhi kama vile, maradhi ya moyo, unene wa maradhi (obesity), kuepuka kupata bawasili, na hata kusaidia mwili kudhibiti kiwango cha sukari katika damu kwa kuchelewesha uyeyukaji wake mwilini. Inadhibiti na kupunguza kiwango cha mafuta  mwilini kwa kuambatana nayo. Na kubwa zaidi huwa ni kinga tosha dhidi ya kansa ya utumbo mkubwa kwani hubeba sumu za kwenye utumbo na kutoka nazo. Kwa lugha isiyo ya kitaalamu labda tunaweza kusema na kumithilisha vyakula vya nyuzinyuzi vinafanyakazi kama brashi. Vinasafisha njia yote ya mfumo wa usagaji chakula.
TIBA
  • Ni pamoja na kunywa maji ya kutosha.
  • Kula vyakula vyenye nyuzinyuzi (fiber), hivi vingi vinapatikana katika mboga za majani, nafaka na matunda.
  • Matumizi ya haluli kama ni tiba inabidi kutumiwa kwa hadhari sana, kwa vile kuzoeleka kwake kunaweza kupelekea uchango ushindwe kufanyakazi wenyewe.
  • Nayo upigaji wa bomba hutumiwa zaidi kama kisisimuzi. Hatahivyo bomba huleta manufaa ama matokeo chanya zaidi pale tu kinyesi kinapokuwa kimejikusanya karibu na mlango wa haja kubwa.
ATHARI ZA MATATIZO YA HAJA KUBWA
Kukosa kupata haja kubwa au ama kupata haja kubwa kwa shida ikiwemo kupata choo kigumu kunaweza kusababisha miongoni mwa maradhi mengine ni pamoja na kupata bawasili, kidonda ama mpasuko katika mlango wa haja kubwa (fisha), kutoka futuru (mwijiko), mrundikano wa kinyesi katika uchango. Hali hii ikiachwa kuendelea tumbo litajaa na kuvimba, litakuwa gumu  na lenye maumivu. Mgonjwa anaweza akawa na dalili za kuziba utumbo yaani kutapika na kadhalika.
HADHARI
Siku zote yapaswa  tuwe makini na tuchukuwe hadhari pale inapotokezea kutopata haja kubwa kwa ghafla na ikadumu kwa siku kadhaa. Hali hii hutokea aghlabu sana kwa wazee na ni moja ya dalili ya kuwepo kwa uvimbe katika uchango mkubwa ambao mara nyingi huwa ni kansa ya utumbo. Bilashaka huambatana na dalili nyengine kama vile kutokwa damu njia ya haja kubwa wakati wa kujisaidia, kuharisha baadhi ya wakati na kupungua uzito wa mwili au kukonda na kadhalika.
USHAURI
Hapanashaka ili kupunguza tatizo hili ambalo linawakabili watu wengi katika jamii yetu, elimu ya chakula bora na mlo ulopangika ndio jibu sahihi ama muarubaini wa kutilia mkazo. Tuanzie skuli na majumbani mwetu kuwaelimisha hasa wanetu. Ni kweli kabisa tumejaaliwa rasilimali nyingi sana  kwa maana ya matunda ya msimu yanayofika kuzagaa kama uchafu na kuharibika, nafaka hadi kuoza ovyo, mboga za majani za kila aina, lakini la ajabu ni kuona watu wetu wengi hawajui thamani ya neema hiyo na kutokuitumia kwake ndio chanzo kikubwa cha maradhi mengi yanayotukabili. Hivyo basi tuwazoweshe watoto wetu kupenda kula matunda, nafaka na mboga za majani tangu wako wadogo, kwani si tu hupelekea kupata haja kubwa kikawaida bali pia vyakula hivi vimejaa vitamini mbalimbali muhimu kwa siha ya mwanadamu.
Muone daktari wako atakuskiliza, atakuchunguza na hatimae atakupa maelezo yenye tija kwako. Tukumbuke samaki mkunje angali mbichi, udongo upate ulimaji.

0 comments:

Post a Comment